Wananchi wa mipakani tushiriki katika ulinzi - Yajayo Yanafurahisha | "Muda Unaongea"

Yajayo Yanafurahisha | "Muda Unaongea"

"Muda Unaongea"

Breaking

Home Top Ad

Post Top Ad

25 Feb 2019

Wananchi wa mipakani tushiriki katika ulinzi

Na Regina Mpogolo.

JUZI Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipotembelea mpaka wa Holili uliopo Tanzania na Kenya katika wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro alisema mpaka huo hauko salama kutokana na kuwapo kwa njia nyingi za panya ambazo wahalifu hutumia kupitisha silaha na bidhaa za magendo. Waziri Mkuu alisema uwepo wa njia nyingi za panya katika mpaka huo inahatarisha usalama wa nchi zote mbili, Kenya na Tanzania na kwamba matukio ya uhalifu yanayoendelea kutokea katika baadhi ya mikoa iliyopo mipakani ni dalili mbaya kwamba mipaka haipo salama.

Pamoja na kwamba Waziri Mkuu aliyataka majeshi ya Kenya na Tanzania kwa kushirikiana na idara za uhamiaji kuanzisha mfumo wa pamoja wa usalama ili kuhakikisha kwamba hakuna mtu anapita na kufanya uhalifu, naamini kwamba wananchi wana jukumu kubwa la kuimarisha ulinzi huo wakishirikiana na majeshi hayo. Watu ambao wanapita katika mipaka hiyo iwe wanaingia hapa nchini au wanatoka kuingia Kenya, kuna watu ambao wanajua mbinu zao lakini wanakaa kimya na kuona kuwa sio kazi yao, ni kazi ya majeshi. Majeshi yetu hayawezi kuwepo kila mahali na kwa wakati wote lakini wanakopita wahalifu hawa iwe ni kwa kupitisha bidhaa zao kwa namna yoyote ile kuna watu ambao huwaona au wanashirikiana nao ambapo wakitoa ushirikiano itasaidia sana. 

Majeshi haya yanahitaji ushirikiano mkubwa kutoka kwa wananchi ili waweze kutokomeza uhalifu ambao unafanyika mipakani au magendo ambayo yanapitia njia za panya katika mipaka yetu. Tukitambua kwamba ulinzi wa nchi ni jukumu letu sote hatutakaa kimya, hata kama ni kwa kutoa taarifa tu kwa mamlaka husika itasaidia kwa kiasi kikubwa kubaini mbinu zao na pia kuwakama. Kuna biashara ambazo pia zinapita katika njia hizi za panya, tukumbuke kwamba bidhaa hizo ndizo ambazo zinaingizwa sokoni bila kulipiwa ushuru wala kodi zozote na kuuzwa kwa bei chini kuliko ile ya kawaida huku nyingine zikiwa katika ubora hafifu au zisizofaa kabisa kwa matumizi. Lakini zikiingia sokoni zinakutana na bidhaa ambazo zimepita njia sahihi, kukaguliwa ubora wake na kuthibitishwa na pia kulipiwa kodi mbalimbali.

Bidhaa hizi mbili zikikutana sokoni wote tunajua nini kinachotokea, watu watakimbilia kununua zile zenye bei nafuu na kuhatarisha afya zao na maisha yao na kuziacha zile zenye ubora. Aidha, kwa kuruhusu kuingiza bidhaa hizi kwa njia za panya inachangia kwa kiasi kikubwa kuua soko la bidhaa za ndani ambazo kiuhalisia zinakuwa na ubora mkubwa. Kuna wananchi ambao wanaishi mipakani lakini hawana uzalendo na nchi yao, wao ndio ambao wanakuwa vinara wa kuwapokea wahalifu na wengine kuficha silaha au bidhaa zao za magendo katika nyumba zao lakini hawatoi taarifa popote.

Ulinzi wa taifa letu uko mikononi mwa kila mmoja wetu kwa kuhakikisha anakuwa mlinzi popote alipo, kuhakikisha kwamba hakuna mbinu chafu itapangwa mbele yake na akakaa kimya bila kuripoti na pia hakuna bidhaa au silaha zitapitishwa kimagendo. Kwa upande wa majeshi yetu ombi kwao watoe ushirikiano mkubwa kwa wananchi wema ambao watajitolea kutoa taarifa za uhalifu wa aina hii, wawe wepesi kupokea taarifa na kuzifanyia kazi mara moja na kwa usiri mkubwa.

Itavunja moyo kama mtu atajitolea kutoa taarifa ya mbinu za uhalifu au ameshuhudia tukio fulani lakini kukawa na uzito wa kufanyia kazi au isifanyiwe kazi kabisa na uhalifu ule ukaendelea na kuathiri watu.

Post Bottom Ad